Wednesday, December 30, 2015








Wednesday, December 30, 2015


Waziri wa Nishati na Madini Profesa Muhongo Aagiza Wala Rushwa Wakamatwe



WAZIRI wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo ameuagiza uongozi wa mkoa wa Kagera,Taasisi ya Kuzuia na Kupamba na Rushwa (Takukuru) na vyombo vya dola, kuwashughulikia wala rushwa katika mradi ya umeme vijijini.

Amezitaka taasisi hizo na uongozi huo, kuchunguza na kuwabaini wanaojihusisha na vitendo hivyo katika mradi huo, unaosimamiwa na Wakala wa Umeme Vijijini (REA), ili wawachukulie hatua ikiwamo kuwafikisha mahakamani.

Alitoa kauli hiyo jana baada ya kupata malalamiko kutoka kwa wananchi na madiwani wanne wa Halmashauri ya wilaya ya Karagwe , wakiongozwa na Mbunge wao, Innocent Bashungwa, ambapo walisema wafanyakazi wa kampuni hiyo wamekuwa wakitoa umeme kwa watu wanaowapatia fedha za pembeni na kusababisha hata ramani ya ufungaji umeme kutofuatwa.

Walisema kwa nyakati tofauti kuwa watu wanaojitambulisha kuwa wanafunga umeme vijijni, wamekuwa wakiwataka wananchi watoe chochote kuanzia Sh 75,000 na kuendelea wakati wameishalipia Sh 27,000 zinazotakiwa kupata huduma hiyo.

Mkuu wa Mkoa wa Kagera, John Mongella alisema amejaribu kufanya utafiti na kugundua kuwa hali hiyo imekuwa ikisababishwa na usimamizi hafifu wa kampuni inayosimamia mradi wa REA.

Wakati huohuo Waziri Muhongo ametaka uongozi wa Shirika la Umeme (Tanesco) mkoa na wilaya ya Karagwe na mkandarasi anayehusika na mradi wa REA, kujibu tuhuma hizo kama wameshazisikia na wamezitatua vipi.

Mhandisi Mshauri wa kampuni ya Urbanand Rural inayoshughulikia ufungaji umeme wa REA eneo hilo, Julius Kateti , alithibitisha kuwepo kwa udanganyifu unaofanywa na baadhi ya wafanyakazi wake wasio waaminifu.

Alisema kutokana na hilo, mpaka sasa ameshawafukuza kazi zaidi ya wafanyakazi 100 kati ya 680 huku kesi nane zikiwa Polisi. 

Baada ya jibu hilo, Muhongo alisema kuwa tatizo hilo limeonekana ni la mkoa mzima na ndipo aliagiza Mkurugenzi wa Usambazaji wa Umeme nchini kutoka REA makao makuu, kufika mkoani Kagera mara moja ili kukaa na uongozi wa Tanesco na wa mkoa wa Kagera kuhakikisha wanatatua masuala hayo.

Meneja wa Tanesco Kanda ya Ziwa, Amos Maganga alimweleza mkandarasi wa REA kuwa ikibainika alichepusha mradi na kupeleka nje ya kilometa 453 za awamu hii kinyume cha mkataba, Tanesco haitatoa fedha ya Serikali kulipia ukiukwaji huo, bali mkandarasi atawajibika mwenyewe.

Akifafanua hilo, Profesa Muhongo alisema serikali imeweka azimio kuwa kampuni itakayobainika kunyanyasa wananchi, haipaswi kupata kazi tena katika awamu zijazo, kwani Watanzania wamechoka na ahadi zisizotekelezeka.
Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )



Wednesday, December 30, 2015

Wizara Ya Kilimo, Mifugo Na Uvuvi Wakemea Tabia Ya Wananchi Kuadhibu Wanyama.

Wizara  ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, imekemea tabia ya kuadhibu wanyama kwenye maeneo ya migogoro baina ya wakulima na wafugaji.

Hayo yalisemwa jana na Mkurugenzi wa Huduma za mifungo Tanzania katika wizara ya Kilimo, mifugo na Uvuvi, Dkt. Abdu Hayghaimo wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

Hayghaimo alisema kuwa wananchi wenye  tabia ya kuwadhuru wanyama waiache mara moja kwa kuwa wanyama hao wanaongozwa na binadamu kwenye maeneo yasiyowahusu wanayama.

Alisema kuwa kwa mujibu wa sheria ya ustawi wa wanyama wanahaki ya chakula, maji, mahali pazuri pakupumzika, kulindwa dhidi ya maumivu yeyote, magonjwa  na mateso ikiwa pamoja na kuwasaabishia kifo.

Pia wizara imewatahadharisha wananchi wote wanaochukua sheria  mkononi na kusababisha madhara makubwa  yasiyokubalika kutokana na migogoro ya migogoro ya wakulima na wafugaji kuwa huwanyima wanyama haki zao ni uvunjifu wa amani.

Jamii imeshauriwa kuwa itafute suruhu ya migogoro hiyo kupitia kamati zitakazo matumizi endelevuya ardhi kwa mujibu wa walaka unaoandaliwa na wizara.
 Toa Maoni Yako( Matusi Hapana )




Wednesday, December 30, 2015

Kampuni Za Simu Zatozwa Faini Kwa Kuwapa AJIRA Raia Wa Kigeni Kinyume Cha Taratibu


Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, anayeshughulikia Kazi, Ajira na Vijana, Anthony Mavunde amebaini kuwepo kwa wafanyakazi wa kigeni, walioletwa na kampuni za simu za mkononi kufanya kazi zinazoweza kufanywa na Watanzania ikiwemo kufunga meza na viti vya kukalia.

Aidha, amebaini kuwepo kwa baadhi ya wafanyakazi wa Kampuni ya simu ya Halotel, raia wa Vietnam, ambao wanaishi nchini bila kibali cha kazi wala cha kuishi. Mavunde aliyabaini hayo jana wakati alipofanya ziara ya kukagua vibali vya ajira kwa wageni, baada ya tangazo lililotolewa na Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu, Jenista Mhagama.

Akiwa katika kampuni hiyo ya Halotel, Mavunde alibaini kuwepo kwa baadhi ya mapungufu, ikiwemo baadhi ya wafanyakazi kutopewa mikataba ya ajira na wenye ajira kutopewa nakala za mikataba yao.

Mavunde aliagiza viongozi wa kampuni hiyo, kuhakikisha kufikia leo wafanyakazi wote wanapewa mikataba huku nakala za mikataba hiyo, ikipelekwa ofisini kwake na pia kuwataka kulipa madeni ya wafanyakazi, hasa madereva, ya saa za ziada (overtime) haraka iwezekanavyo.

“Tumegundua kuwepo kwa mapungufu mengi katika kampuni yenu, hii ni pamoja na wafanyakazi wenu kutojiunga katika mifuko ya hifadhi ya jamii na kumekuwa na makato ambayo hayapo kwa mujibu wa sheria za kazi.

"Lakini pia kuna wageni ambao wako katika hii kampuni yenu, wanafanya kazi ambazo zinaweza kufanywa na Watanzania, kwa mfano huyu anayefunga viti, hii kazi inafanywa na vijana wetu…kibali chake kinaisha kesho, naagiza asipewe kingine na aondoke,” alisema Mavunde.

Aidha, alisema katika masuala ya usalama mahali pa kazi, pia kuna mapungufu mbalimbali, ikiwemo wafanyakazi kutopewa mafunzo ya kukabiliana na majanga, vipimo vya afya na makosa mengine ambapo kwa mujibu wa sheria aliwatoza faini ya Sh milioni sita.

Hata hivyo, wakati akiendelea kutoa maagizo hayo, mmoja wa maofisa wa Ubalozi wa Vietnam, Mai Anh Thai aliingia katika ukumbi wa mkutano na kutaka kumkatisha Naibu Waziri kwa madai kuwa hakufuata utaratibu.

Kutokana na kuchafuka kwa hali ya hewa huko, ilimlazimu Mshauri wa kampuni hiyo ambaye jina lake halikuweza kupatikana mara moja, kumshauri ofisa huyo taratibu za ukaguzi zilivyo.

Baada ya kutoka katika kampuni hiyo, Mavunde na maofisa wa Uhamiaji, Wizara ya Kazi, Ajira na Vijana na askari walilazimika kufika katika nyumba ambayo iko Mikocheni, ambako inasadikiwa kuwa wapo raia wengi wa Vietnam wanaoishi hapo, huku wengine wakiwa hawana vibali vya kuishi wala vya kazi.

Walipofanya msako katika nyumba hiyo, baadhi ya raia hao walijificha na kufanikiwa kumkamata mmoja ambaye hakuwa na kibali chochote. Hata hivyo, mmoja wa walinzi wa nyumba hiyo alisema raia hao walikuwa wengi, lakini baadhi yao walitoroshwa juzi usiku.

Awali akiwa katika Kampuni ya Airtel, Mavunde aliwapiga faini ya Sh milioni nne kutokana na kuwepo na mapungufu mbalimbali katika masuala ya usalama na afya mahali pa kazi, ambazo wanapaswa kulipa ndani ya siku 14.

Aidha, aliwataka waajiri nchini kote, kuhakikisha wanasimamia sheria za kazi ili kujenga nchi ambayo haina misuguano. Mavunde alionya kuwa wanaobeza kuwa hiyo ni ‘nguvu ya soda’, wafute jambo hilo, kwani kazi hiyo ni endelevu.
Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )




Wednesday, December 30, 2015

Waziri Mkuu Atembelea Kambi za Wakimbizi Kigoma.....Awaonya Kutobeba Silaha Wanapoingia Nchini, Ataka walionazo wazisalimishe

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewaasa raia wanaokimbia nchi zao na kupata hifadhi Tanzania kutobeba silaha wanapoingia nchini kuja kuishi kwenye kambi za wakimbizi.

Ametoa onyo hilo jana  wakati akizungumza na mamia ya wakimbizi wanaoishi kwenye kambi za Nyarugusu na Nduta zilizoko wilayani Kasulu na Kibondo, mkoani Kigoma waliofika kumsikiliza kwenye mikutano ya hadhara iliyofanyika kwenye kambi hizo.

“Ninawasihi mjitambue kuwa mmehama kutoka DRC na Burundi, na mnapoingia hapa inabidi mbadilike muwe na tabia za hapa. Hatuhitaji mje na silaha au vifaa hatarishi kwa sababu tunataka mkae kwa usalama,” alisema.

Alisema suala la usalama ni muhimu miongoni mwao, ni muhimu zaidi kwa majirani zao lakini pia ni muhimu sana kwa watoa huduma wanaowahangaikia. 
“Tunataka kila mmoja awe mlinzi wa mwenzake ili siku mkiondoka mrudi nyumbani mkiwa salama,” alisema.

“Ninyi mko hapa mnatunzwa kwa hiyo hamruhusiwi kutoka kambini na kutembea hovyo huko nje. Hii ni kwa usalama wenu. Hatumruhusu kuingia na bunduki au mabomu na yeyote atakayemuona mwenzie ana silaha au ameificha mahali aje atuambie ili tumchukulie hatua na ninyi wengine mbakie salama,” alisisitiza.

Kuhusu maambukizi ya Virusi vya UKIMWI (VVU), Waziri Mkuu aliwataka wakimbizi hao wajiepushe na ngono zembe kwa sababu kiwango cha maambukizi kimeongezeka kwa asilimia moja ikilinganishwa na mwaka jana

“Nimetembelea hospitali yenu hapa kambini na kuelezwa kuwa maambukizi ya VVU hapa yapo na mwaka huu yamefikia asilimia mbili ya watu waliopimwa ikilinganishwa na mwaka ambapo ilikuwa ni asilimia moja tu,”

“Kutokana na uwingi wenu, naomba niwasihi sana mjizuie kufanya ngono zembe na kama mtu atashindwa kabisa kujizuia ni vema atumie kinga. La sivyo mtaleta maambukizi ya juu sana na wote mtakwisha,” alisema.

“Suala lenyewe siyo jambo la dharura, kawaida huwa kuna maandalizi baina ya wahusika, watu wanakubaliana juu ya muda na mahali pa kukutana ndiyo maana nasema siyo jambo la dharura. Ndugu zangu tujihadhari sana kwa sababu kasi ya maambukizi mahali hapa iko juu sana,” alisisitiza.

Mapema, Mkuu wa kambi ya Nyarugusu, Bw. Sospeter Boyo alimweleza Waziri Mkuu kwamba kambi hiyo ilifunguliwa Novemba 1996 kwa lengo la kuwahifadhi wakimbizi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo waliokuwa wakikimbia vita ya wenyewe kwa wenyewe.

Alisema kambi hiyo yenye ukubwa wa kilometa za mraba 28, ina uwezo wa kuhifadhi wakimbizi 50,000 lakini kwa sasa inao wakimbizi 151,032 ambao ni mara tatu zaidi ya uwezo halisi wa kambi hiyo.

“Tangu Aprili mwaka huu, idadi ya wakimbizi imeongezeka hadi kufikia 151,032 miongoni mwao ni wakongo 61,313, warundi 89,619, Wanyarwanda 75, Waganda 12, Wasudan kusini wane,Wakenya wane, Msomali mmoja, Mzimbabwe mmoja na raia wa Ivory Coast mmoja,” alisema Bw. Boyo.

Alisema wanakabiliwa na changamoto za uhaba wa maji safi, ufinyu wa huduma za afya na elimu na uharibifu wa mazingira.

Waziri Mkuu bado anatembelea pia kambi ya JKT ya Mtabila wilayani Kasulu na kesho asubuhi ( leo) anatarajiwa kufanya majumuisho ya ziara yake.
 
IMETOLEWA NA:

OFISI YA WAZIRI MKUU,

JUMANNE, DESEMBA 29, 2015.
Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )










MWENEBATO

Wednesday, December 30, 2015


 Mh: Lukuvu Aagiza Watumishi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kufanya kazi hadi Usiku, Abaini Urasimu Mkubwa Wizarani


Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi amewaagiza watumishi wa wizara hiyo katika kitengo cha huduma kwa wateja, kufanya kazi hadi usiku ili kuhakikisha wanawahudumia kwa muda wananchi wengi wanaofika katika kitengo hicho na kuondoka bila kupata huduma stahiki.

Waziri Lukuvi alitoa maagizo hayo jana alipofanya ziara katika kitengo hicho na kubaini kuwepo urasimu mkubwa unaopelekea wananchi kushindwa kupata huduma kwa wakati. 

Baada ya kuzungumza na baadhi ya wananchi waliofika katika kitengo hicho, alibaini kuwepo wananchi ambao wamekuwa wakifuatilia hati zao kwa takribani miezi mitatu bila mafanikio lakini alipoagiza wapewe hati hizo zilipatikana mara moja.

“Watu wasirudi bila kuhudumiwa. Na kama ni wafanyakazi watabaki mpaka usiku, tutafanya utaratibu wa hao wafanyakazi wanaobaki mpaka usiku. Wafanyakazi wabaki muda zaidi lakini kila anayekuja katika kituo kile lazima ahudumiwe,” alisema Lukuvi.

Pia, Lukuvi aliagiza kufungwa kwa mitambo itakayosaidia kutoa huduma za kieletroniki. Alisema kuwa uanzishwe mfumo wa kuwasiliana na wananchi wanaohitaji huduma katika kitengo hicho kwa njia ya barua pepe, whatsap, simu na kadhalika.

Naye Kaimu Katibu Mkuu wa wizara hiyo ambaye pia ni kamishna Mkuu wa ardhi, Dk Moses Kusiluka alisema kuwa katika utoaji wa huduma hukutana na changamoto inayotokana na baadhi ya watu wanaotaka kujipatia hati kwa njia za udanganyifu bila kuwa na nyaraka za kisheria husasan wanapokuja kuwawakilisha watu wengine.
Tupe Maoni Yako( Matusi Hapana )


Tuesday, December 29, 2015

Kizingiti mazungumzo ya amani Burundi


Mazungumzo ya kujaribu kutafutia ufumbuzi mzozo wa kisiasa nchini Burundi yamefanyika nchini Uganda.
Hata hivyo washiriki wamekosa kuelewana kuhusu siku ya kuanza kwa mazungumzo kamili.
Majadiliano hayo, yaliyoongozwa na Rais wa Uganda Yoweri Museveni, yalikuwa ya kuweka mikakati ya kufanyika kwa mazungumzo ya kina kuhusu mzozo nchini humo.
JanuariMachafuko yalianza Burundi baada ya Rais Pierre Nkurunziza kutangaza nia yake ya kuwania uchaguzi kwa muhula wa tatu.
Alishinda uchaguzi huo uliofanyika Januari.
Mkutano huo uliafikia mazungumzo ya kina yaanze Januari 6 mjini Arusha, Tanzania lakini ujumbe wa serikali ya Burundi umesema hakukuwa na “makubaliano kuhusu tarehe hiyo”.
Msemaji wa afisi ya rais wa Burundi Willy Nyamitwe alitoa taarifa kwa vyombo vya habari baada ya mazungumzo ya leo akipinga tarehe hiyo.
Mazungumzo hayo yamefanyika katika ikulu ya rais wa Uganda mjini Entebbe.
Rais Museveni, aliyeteuliwa na viongozi wa kanda kuongoza mazungumzo hayo, ametoa wito kwa upande wa serikali kutochukua msimamo mkali.
"Wanaweza kuwa wahalifu lakini kwa sababu za kuleta amani wacha watu hawa tuwape kinga ya muda. Hata nyinyi wakati ule mlikuwa mnavunja haki za binadamu (mlipokuwa waasi), kama vile kuua raia wa kawaida,” amesema.
Burundi
Bw Museveni ameitaka serikali ya Burundi kutotoa masharti makali
“Huo ni uhalifu wa kivita hata mkiwa waasi. Mkiwa waasi kuweni waasi wazuri, msiwe waasi wabaya kwa kuwaua raia ambao si askari. Unaweza kutenda uhalifu wa kivita ukiwa serikalini au upande wa upinzani.”
Muungano wa Afrika umesema unapanga kutuma walinda amani 5,000 nchini humo, hatua ambayo imepingwa na serikali ya Burundi.
Waziri wa mashauri ya kigeni wa Burundi Alain-Aime Nyamitwe aliongoza ujumbe wa serikali kwenye mazungumzo hayo.
Awali naibu kwanza wa mwenyekiti wa chama tawala cha CNDD FDD Victor Burikukiye alikuwa ametoa masharti kadhaa ikiwemo kutokubali kukaa katika meza moja na "wauaji waliopanga mapinduzi ya kijeshi yaliyofeli”.
Kulikuwa pia na wawakilishi kutoka vyama vya upinzani na makundi ya kiraia.

Friday, August 28, 2015

Picha za Mafuriko ya Magufuli Sumbawanga


...
Read More

Magufuli Akataa Mawaziri Wazembe......Asema Serikali Yake Haitakuwa na BlaaBlaa Katika Utendaji Kazi

Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli, amesema serikali yake ya awamu ya tano haitakuwa na blablabla katika utendaji wa kazi na kuonya kuwa waziri atakayeshindwa kutelekeza majukumu yake, ataondolewa ili kupisha wenye uwezo. Dk.  Magufuli alitoa ahadi hiyo jana, wakati akijinadi kwa wananchi wilayani Nkasi na Kalambo,