Friday, February 5, 2016

My Heart Is Crying for You (Official Gospel Audio) ~ by John Bera




Thursday, February 4, 2016


Serikali Yalaani Kitendo Cha Kudhalilishwa Kwa Mtanzania Nchini India

Serikali ya Tanzania imesikitishwa na inalaani vikali kitendo cha udhalilishwaji alichofanyiwa mwanafunzi wa kike wa Kitanzania na Kundi la watu katika jimbo la Bangalore nchini India.

Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Balozi Ramadhani Muombwa Mwinyi alipokutana na Wandishi wa Habari kwa ajili ya kuwaeleza hatua zilizochukuliwa na Serikali kufuatia kitendo hicho cha kudhalilishwa kwa mwanafunzi wa Kitanzania nchini India.
 
Balozi Mwinyi alisema kuwa, hatua zilizochukuliwa ni pamoja na Ubalozi wa Tanzania nchini India kuiandikia Serikali ya nchi hiyo kuomba maelezo kamili kuhusu tukio hilo pamoja na kuitaka Serikali ya India kuwachukulia hatua za kisheria watu wote waliohusika pamoja na kuimarisha usalama katika maeneo wanayoishi wanafunzi wa Kitanzania. 
 
Aidha, Balozi Mwinyi alieleza kuwa amemwita Balozi wa India hapa nchini, Mhe. Sandeep Arya na kumweleza masikitiko ya Serikali ya Tanzania kufuatia kitendo hicho cha kushambuliwa na kudhalilishwa kwa mwanafunzi wa kike kutoka Tanzania.
 
Katika mazungumzo yao, Balozi Arya alieleza bayana kuwa Serikali ya India imesikitishwa na tukio hilo la udhalilishaji na kwamba Serikali imeahidi kuwachukulia hatua za kisheria wale wote watakaobainika kutekeleza uovu huo.
 
Alisema kuwa Waziri Mkuu wa Jimbo la Bangalore aliongea na umma kuelezea masikitiko yake kuhusu uovu huo na kuahidi kuwa mamlaka za jimbo hilo zitaimarisha usalama katika maeneo yote wanayoishi wanafunzi wa Tanzania na raia wengine kutoka nje.
 
Balozi Arya aliihakikishia Serikali ya Tanzania kuwa India inaheshimu ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na nchi yake, hivyo itashughulikia suala hilo kwa ukamilifu na hadi wakati huu tayari watu watano wanashikiliwa na vyombo vya usalama wakituhumiwa kuhusika na tukio hilo.

Sanjari na taarifa hiyo, Balozi Mwinyi aliwaomba Watanzania kutohusisha tukio hili la uhalifu na ajali ya Mtanzania, Bw. Christian Benjamin Mlyansi iliyotokea nchini India jana usiku na kusababisha kifo chake.
Alisema kuwa Bw. Mlyansi alipata ajali ya kawaida alipokuwa anaendesha pikipiki ambapo ilipoteza mwelekeo na kugonga ukingo wa kati wa barabara.



Thursday, February 4, 2016

Mke wa Kafulila atimuliwa nje ya ukumbi wa bunge

Mbunge wa Viti maalum Chadema Jesca Kishoa ametolewa nje ya ukumbi wa bunge na kutakiwa kutohudhuria vikao viwili vya bunge linaloendelea mjini Dodoma.

Hayo yamejiri katika mkutano wa 7 wa bunge la 11 linaloendelea na vikao vyake mjini Dodoma ambapo Mwenyekiti wa kikao cha leo Andrew Chenge amelikumbusha bunge kuhusiana na kauli aliyoitoa mbunge huyo tarehe 01/02/2016.
  
Mbunge huyo alisema kwamba Waziri Harrison Mwakyembe alihusika kununua mabehewa feki 274 jambo ambalo lilizua mjadala mkali na bunge kumtaka mbunge huyo atoe ushahidi ndani ya siku 3.

Mwenyekiti Andrew chenge amesema kuwa mbunge huyo alitakiwa kwa mujibu wa kanuni za bunge kanuni ya 63(6) atoe ushahidi kwa ofisi ya bunge na ndani ya siku zote ofisi ya bunge haijapata ushahidi huo.

Kutokana na Mbunge huyo ambaye pia ni mke wa aliyekuwa mbunge wa Kigoma kusini David Kafulila NCCR Mageuzi kushindwa kutekeleza maamuzi ya bunge mwenyekiti wa bunge amemtaka kufuta kauli yake na mbunge huyo akakaidi ndipo Mwenyekiti akamuamuru atoke nje mara moja na kutohudhuria vikao vya bunge kwa siku zilizobakia 2.
Friday, February 5, 2016

Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Ijumaa Ya Februari 5


Friday, February 5, 2016

CT-Scan Iliyopelekwa Muhimbili Ilikuwa Ya UDOM


WIZARA ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto imekiri kwamba mashine ya CT Scan iliyofungwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili ilikuwa ni ya kituo cha kisasa cha kutolea huduma za afya cha Benjamin Mkapa kilichopo katika Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).

Akijibu swali la nyongeza bungeni mjini Dodoma, Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Khamis Kigwangalla alisema mashine hiyo iliingia nchini kwa lengo la kupelekwa katika kituo hicho lakini ikapelekwa Muhimbili kutokana na kutokamilika kwa majengo ya kufungwa mashine hiyo katika kituo hicho.

Alisema, uamuzi huo waliuchukua pia kwa sababu hela ya kununua mashine nyingine ambayo itapelekwa kufungwa katika kituo hicho ilikuwepo na kwa sasa mchakato wa ununuzi unaendelea.

Dk Kigwangalla alikuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Chemba, Juma Nkamia (CCM) aliyetaka jibu la Serikali kama ni kweli ilichukua mashine ya kituo hicho na kufunga katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ama ilinunua.

Awali katika swali la msingi msingi, Nkamia alitaka kujua mpango wa Serikali wa kununua mashine mpya ya CT -Scan kwa ajili ya Hospitali ya Taifa Muhimbili.
 Kuhusu hilo, Dk Kigwangalla alisema, Desemba mwaka jana Serikali ilipeleka mashine ya CT-Scan katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili ambayo inatumia teknolojia ya kisasa yenye X-ray tube mbili na uwezo wa kupiga picha ya 128 slice mara mbili.

Friday, February 5, 2016

Serikali Yajieleza Bungeni Kinachosababisha Umeme Ukatike Mara Kwa Mara


Serikali  imesema tatizo la kukatika kwa umeme mara kwa mara nchini linatokana na uchakavu na kuzidiwa kwa vituo vya kupoza umeme na miundombinu ya usafirishaji na usambazaji nishati hiyo.

Katika kukabiliana na tatizo hilo Tanesco inachukua hatua za kujenga mifumo ya njia kubwa za umeme wa msongo wa kilovoti 400 (Iringa- Dodoma-Singida-Shinyanga), gridi ya Kaskazini Mashariki (Dar es Salaam, Chalinze,Tanga –Arusha), ya Kaskazini Magharibi (Geita- Kagera –Katavi- Kigoma- Rukwa na Mbeya) na Makambako- Songea wa kilovoti 220.

Kauli hiyo ilitolewa bungeni jana na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dk Medard Kalemani wakati akijibu swali la Mbunge wa Magu, Boniventure Kiswaga (CCM). 
Kiswaga alitaka kufahamu serikali imejipangaje kukabiliana na tatizo la kukatika katika kwa umeme.

Pia mbunge huyo alitaka kufahamu, Je serikali itakamilisha lini kupeleka umeme katika vijiji vya jimbo hilo ikizingatiwa mpaka sasa ni asilimia 20 tu ya vijiji ndiyo vina umeme. 
Kalemani akijibu swali hilo, alisema tatizo la kukatika kwa umeme linatokana na uchakavu na kuzidiwa kwa miundombinu ya kupoza umeme pamoja na matukio ya kulipuka kwa transfoma yanayosababishwa na radi hasa kipindi cha mvua pamoja na wizi wa mafuta ya transfoma unaofanywa na wananchi wasio waaminifu.

Alisema Tanesco inakamilisha upanuzi wa usambazaji wa umeme katika majiji makubwa ya Arusha, Dar es Salaam, na Mwanza ambapo kazi hizo zitahusisha ujenzi wa njia mpya za umeme na kupanua vituo vya kupoza umeme.

“Kukamilika kwa kituo cha kupoza umeme cha KIA mkoani Kilimanjaro kumeimarisha upatikanaji wa umeme maeneo ya Mirerani na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA),” alisema Kalemani.

Pia vituo vya kupoza umeme katika jiji la Dar es Salaam vya Gongo la Mboto, Kipawa, Mbagala, na Kurasini vitaunganishwa kwa njia ya sakiti mzunguko kutoka Ubungo na Kinyerezi kuanzia Machi mwaka huu.

Friday, February 5, 2016

Rais Magufuli Asema Yeye si Kichaa wala Dikteta......Aahidi Kuifanyia Mema Nchi hata Akifa awe Rais wa Malaika

RAIS Dk. John Magufuli amesema anapochukua hatua yeye si kichaa, si dikteta, si shetani wala si mnyama, ila ni mpole, lakini amefika mahali lazima afanye hivyo kwani ndani ya Serikali yanafanyika mambo ya ajabu.

Kauli hiyo aliitoa jana jijini Dar es Salaam katika kilele cha Siku ya Sheria nchini, alipokuwa mgeni rasmi kwa mara ya kwanza katika uzinduzi wa Mwaka wa Mahakama tangu alipoapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Alisifu kazi kubwa inayofanywa na Idara ya Mahakama, huku akitangaza uamuzi wa gharama za kurusha matangazo ya moja kwa moja ya Bunge zaidi ya Sh bilioni nne ni bora zikawasaidia wananchi.

“Ninapochukua hatua mimi si mnyama, si dikteta, si shetani, ni mpole kweli, lakini inafika mahali lazima nifanye, yanayofanyika serikalini ni mambo ya ajabu sana, nataka kutoa sadaka yangu, inawezekana hata nikifa naweza kuwa rais wa malaika,” alisema.

Alipongeza kazi kubwa inayofanywa na mahakama huku akibaki kujiuliza kwanini katika maadhimisho ya siku yao hawarushi matangazo yao moja kwa moja kupitia luninga.

“Mnafanya kazi kubwa, nilipofika niliuliza kwanini hii siku yenu hamrushi ‘live’, nikajibiwa fedha za kurusha ‘live’ zinapelekwa kuwahudumia wananchi.

“Kipindi kimoja kurusha ‘live’ kwa wiki mbili inatumika zaidi ya Sh bilioni nne, ni vizuri kuzikata hizo fedha zinazopelekwa kurusha ‘live’ zikapelekwa katika kesi za ubunge zinazohitaji shilingi bilioni tatu kusikilizwa hadi kumalizika kwake,” alisema.

Alisema mahakama ilikuwa inapewa bajeti ya Sh bilioni 41, lakini mwaka 2015/2016 ilishuka wakatakiwa kupewa Sh bilioni 12 ambazo hadi sasa hawajapewa.

“Kiongozi lazima ufikirie wapi pa kupeleka fedha na wapi pa kunyima, watu wa mahakama mnafanya kazi ya Mungu, nawaahidi ndani ya siku tano nitakuwa nimewapa Sh bilioni 12 zote.

“Sina tatizo la masilahi ya wafanyakazi wa mahakama, katika bajeti ya mwaka huu nitawapa fedha nyingi kuliko bajeti zote zilizopita, fedha zipo,” alisema.

Mahakimu Kutumbuliwa
Rais Magufuli alisema anamwagiza Jaji Mkuu kuwachukulia hatua mahakimu 502 ambao hawakufikia malengo ya kumaliza kesi 250-260 kwa mwaka. Walimaliza kesi chini ya 100.

“Mahakimu ambao hawajafikia kumaliza kesi 260 hayo ndiyo majipu yako Jaji Mkuu, unatakiwa kuyatumbua, wewe uliniapisha hata mimi, leo unapitisha agizo mwingine anapinga.

“Unatoa siku saba sasa sijui ndiyo watamaliza kutoa hizo hukumu, nakuagiza wachukulie hatua, tusipochukua hatua hakuna kitakachofanyika.

“Walioshindwa kufikia lengo unawabakiza wa nini, wasomi wako wengi, hata ukitangaza leo watajitokeza, niruhusu mimi nitangaze, sitaki kuingilia mahakama,” alisema.

Mabilioni ya NIDA
Akizungumzia hatua yake kwa watendaji wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), alisema ilipewa Sh bilioni 176.6, lakini vitambulisho vilivyotengenezwa havifiki hata milioni mbili na havina sahihi wakati vitambulisho vya kupigia kura fedha iliyotolewa haizidi Sh bilioni 70, lakini vina sahihi za wapigakura wote wa Tanzania ambao ni milioni 23,253,982.

“Utaona ugumu wa kuongoza, nchi inatawaliwa na madudu ya kila aina, wapo watu wanacheza na fedha wanavyotaka wakati wapo watu masikini sana, wengine wanataka bodi zao wakakae Ulaya.

“Hapo ndipo tulipofikia, wengine wanalipwa mshahara kwa mwezi Sh milioni 35, naomba mniombee kabla ya kunihukumu, toeni hukumu kwa haki kwa hawa wanaotaka kuifikisha nchi pabaya, toeni hukumu zao haraka,” alisema.

Kesi za Wakwepa kodi
Rais Magufuli alisema kuna kesi 442 za kukwepa kodi ambazo zingeamuliwa Serikali ingepata Sh trilioni moja, ambayo ingeweza kununua ndege zaidi ya sita.

Alimuomba Jaji Mkuu kuzimaliza kesi 442 na kama zikimalizika fedha hizo Sh trilioni moja ataipa Idara ya Mahakama Sh bilioni 259 na Sh bilioni 750 zilizobakia zitanunuliwa ndege sita na wafanyafakazi 250 ATCL waliopo sasa wataondolewa.

Akizungumzia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, alisema kuna kesi 26 za watu waliokutwa na nyara za Serikali, ambazo zipo zaidi ya miaka mitano hazijaamuliwa kwa sababu upelelezi bado.

“Polisi wapo, DPP yupo, upelelezi unaendelea kila siku, hapo unaona tatizo lilipo, DPP upo unapeleleza nini au unatafuta rushwa?” alisema.

Alisema suala la kuanzishwa kwa mahakama ya mafisadi ya wahujumu uchumi halihitaji kwenda bungeni kufanya mabadiliko, lifanywe haraka, mahakama ianze kwani nchi inachezewa.

Pamoja na hali hiyo Rais Magufuli alikubali kupokea maombi yote yaliyotolewa na mahakama na kuyazingatia kwani lazima ayaunge mkono ikiwamo kukubali watumishi wa Idara ya Mahakama wasome na kupatiwa mikopo na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB).

“Nimeamua nchi iende na itaenda, anayefikiria ataikwamisha atakwama yeye, nategemea zaidi mahakama katika kufanikisha hilo,” alisema.