Tuesday, March 8, 2016

Tuesday, March 8, 2016

Stephen Wasira Amng’ang’ania Ester Bulaya......Wapiga Kura Wanne Wanaompigania Wawasilisha Upya Ombi la Kukata Rufaa



Wapigakura wanne wa Jimbo la Bunda Mjini mkoani Mara, wamekamilisha taratibu za kimahakama na kuwasilisha upya maombi ya kukata rufaa katika Mahakama ya Rufaa ya Tanzania kutokana na maombi yao ya awali kutupiliwa mbali Februari 24, mwaka huu.

Maombi hayo yamewasilishwa na wapigakura Magambo Masato, Matwiga Matwiga, Janes Ezekiel na Ascetic Malagila dhidi ya Mbunge wa Bunda Mjini, Ester Bulaya, kuiomba mahakama hiyo kuwapa kibali cha kukata rufaa katika mahakama hiyo.

Wapigakura hao ambao wamekuwa wakimpigania aliyekuwa Waziri wa Chakula, Kilimo na Ushirika na mgombea ubunge wa CCM Jimbo la Bunda Mjini, Stephen Wasira, waliwasilisha maombi ya kufungua shauri katika Mahakama ya Rufaa ya Tanzania ili itoe ufafanuzi kuhusu haki ya mpigakura ya kuhoji matokeo pamoja na vigezo vinavyotakiwa ili aweze kuhoji matokeo ya uchaguzi.

Maombi yao ya awali yalitupiliwa mbali na Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Sirilius Matupa kutokana na kuwasilishwa sura 141 ya sheria ya rufaa na kueleza kuwa yalikuwa yamewasilishwa chini ya kifungu cha 15 (a) (b) badala ya kifungu 15 (c) ambacho ndiyo sahihi kwa ajili ya maombi hayo na kuwaeleza wanaweza kurekebisha na kuyawasilisha upya.

Januari 25, mwaka huu Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Mohamed Gwae, aliitupilia mbali kesi namba moja ya kupinga matokeo ya Uchaguzi Jimbo la Bunda Mjini iliyofunguliwa na wapigakura hao dhidi ya Bulaya.

Wakati huo huo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Sumbawanga, Kakusulo Sambo anayesikiliza kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi Jimbo la Nyamagana, amekutana na mawakili wa pande zote na kuweka mikakati ya namna ya kuiendesha.

Jaji Sambo amekutana jana na mleta maombi (Ezekiel Wenje), mjibu maombi wa kwanza (Stanslaus Mabula) pamoja na mawakili wanaowawakilisha kuweka mikakati ya uendeshwaji wa kesi hiyo ikiwa ni pamoja na kubainisha sehemu zinazobishaniwa.

Akizungumzia hatua hiyo, Wakili Deya Outa anayemwakilisha Wenje, alisema katika kikao hicho wamebainisha sehemu zinazobishaniwa na pande zote katika kesi hiyo pamoja na mashahidi watakaotakiwa kufika mahakamani kutoa ushahidi.
==

Friday, March 4, 2016


Friday, March 4, 2016

Taarifa Fupi Kuhusu Ziara Ya Rais Wa Vietnam Nchini Tanzania Tarehe 9-10 Machi 2016


Utangulizi
Rais wa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Vietnam Mheshimiwa Truong Tan Sang anatarajiwa kufanya ziara rasmi nchini tarehe 9 Machi 2016.  
Madhumuni ya  ziara hiyo ni kukuza uhusiano baina ya Vietnam na Tanzania mbao umedumu kwa zaidi ya miaka hamsini tangu kuanzishwa kwake pamoja ‎Kufungua maeneo mapya ya Ushirikiano wa kiuchumi baina ya Tanzania na Vietnam. 
Hii ni ziara ya kwanza ya kiongozi huyo Barani Afrika tangu aingie madarakani mwaka 2011, ambapo nchi nyingine anayotarajiwa kutembelea ni Mozambique. 
Rais Truong anatarajiwa kufuatana na mke wake Bi Mai Thi Hahn, mawaziri 4 wanaoshughulika na sekta za  Kilimo, Mawasiliano Uwekezaji, Afya,Viwanda na Biashara.  Aidha mgeni huyo atafuatana na ujumbe wa wafanyabiashara 30 kutoka Vietnam. 

Shughuli za msingi zitakazofanyika kwenye ziara
Wakati wa ziara hiyo Rais Truong Tang San atafanya mazungumzo rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dk. John Pombe Joseph Magufuli Ikulu jijini Dar-es-Salaam.
 
Aidha, Rais Truong pia atapata fursa ya kutembelea eneo la EPZ la Ubungo kuangalia viwanda mbalimbali vinavyozalisha bidhaa za kuuza nje
 
Baada ya kutembelea EPZA Rais Truong atahudhuria mkutano wa biashara na uwekezaji katika ukumbi wa mikutano wa Julius Nyerere. Mkutano huo unatarajiwa kuhudhuriwa na taasisi za umma na sekta binafsi kutoka Tanzania na Vietnam.
 
Rais Truong atamaliza ratiba yake kwa kuhudhuria dhifa ya Taifa itakayoandaliwa kwa heshima yake na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dk.John Pombe Joseph Magufuli.

Wasifu wa Rais wa Vietnam‎
M‎heshimiwa Truong Tan Sang amezaliwa tarehe 21 January 1949 katika Jimbo la Long An nchini Vietnam. Amepata Elimu ya Juu kutoka taasisi ya national Academy of Public Administration ya Vietnam ambako alipata Shahada ya kwanza ya Sanaa na Sheria.
 
Kutokea mwaka 1966 hadi 1996 Mheshimiwa Truong ameshika nafasi mbalimbali za utendaji  katika Chama Tawala cha kikomunisti cha Vietnam.
 
Mwaka 1996 Mhe Truong alichaguliwa kuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama Tawala na Katibu wa Chama hicho katika Jimbo la Ho Chi minh hadi mwaka 2000 ambapo aliachia wadhifa wa katibu Mkuu wa Jimbo na kuendelea na nafasi ya ujumbe wa Kamati kuu ya Chama tawala hadi tarehe 25 Julai 2011 alipochaguliwa na Bunge la Vietnam kuwa Rais wa Vietnam.
 
Mhe Truong amemuoa Bi mai Thi Hanh  na wamejaaliwa mtoto mmoja.

Taarifa Muhimu Kuhusu Vietnam‎
Historia fupi ya Vietnam
Vietnam ilifanya mapinduzi tarehe 14 Agosti 1945 na hatimaye kupata uhuru tarehe 2 Septemba 1945 ikijulikana kwa jina la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Vietnam. 
Pamoja na kupata uhuru nchi hiyo iliendelea kuwa na migongano baina ya Vietnam ya Kaskazini na Kusini iliyopelekea vita iliyodumu kwa muda mrefu na kuhusisha mataifa ya nje. 
 
Kufuatia kumalizika kwa vita, Vietnam ya Kaskazini na Kusini ziliungana tena na kuunda Jamhuri ya Kisoshalisti ya Vietnam tarehe 2 Julai 1976. 
Nchi hiyo yenye kilomita za mraba 329,560 iliyopo kusini mashariki mwa Asia ina watu milioni 91.7 na inaongozwa na Chama cha Kikomunisti cha Vietnam.

Mafanikio ya Uchumi ya Vietnam
‎Vietnam ni moja ya nchi zilizopiga hatua kubwa ya maendeleo barani Asia.
Mwaka 1986 Serikali ya Vietnam ilianzisha mageuzi makubwa ya uchumi yaliyopelekea kuitoa nchi hiyo kwenye kundi la nchi masikini yenye kipato cha Dola za Kimarekani 100 kwa kila mtu hadi kufikia kuwa nchi yenye uchumi wa kati yenye kipato cha Dola za kimarekani 2000 kwa kila mtu mwaka 2014. Katika mageuzi hayo,Vietnam imefanikiwa kupunguza umasikini wa wananchi wake kwa asilimia 50.

Mafanikio katika Sekta ya Kilimo
Sifa kuu ya Vietnam ni uthubutu na uwezo wa kusimamia mipango yake. Mfano mwaka 1980 nchi hiyo iliamua kuingia kwenye uzalishaji mkubwa wa kahawa. 
Ndani ya miaka 10 iliweza kufikia uzalishaji wa tani 300,000 kwa mwaka na hatimaye kuwa nchi inayoongoza ulimwenguni katika uzalishaji na uuzaji wa kahawa aina ya Robuster. 
Vilevile miaka ya 1990, Vietnam ilikuwa ikiagiza mchele kutoka nje, kufuatia hatua madhubuti walizochukua mwaka 2004 ilishika nafasi ya pili duniani katika uzalishaji wa mchele kwa kuwa na misimu mitatu ya mavuno.
 
Hivi sasa Vietnam imejiwekea malengo ya kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa sukari duniani ambapo mwaka 2015 uzalishaji wake umefikia tani milioni 2 kwa mwaka.‎ 
Mbali na mazao hayo, Vietnam inaongoza ulimwenguni kwa kuuza korosho na pilipili manga. Vilevile,Vietnam ni miongoni mwa nchi zinazoongoza kwenye kilimo cha muhogo na mpira. 
  ‎
Mafanikio makubwa ambayo Vietnam imeyapata katika kuongeza uzalishaji katika sekta ya kilimo, yamekuwa chachu ya ukuaji wa sekta ya viwanda ambayo kwa sasa ndio imeshika hatamu ya uchumi wa Vietnam‎.
 
Mkakati wa Mageuzi ya Kijamii na Kiuchum 2011-2020
Aidha, Vietnam inatekeleza mkakati wake wa kuwezesha mageuzi ya kijamii na kiuchumi wa mwaka  2011-2020 ambao umejikita kwenye kuwapatia wananchi elimu na stadi za ufundi‎ kwa ajili ya kufanya kazi kwenye viwanda vinavyotumia teknolojia ya kisasa na ubunifu; kuboresha taasisi zinazoshughulika na masoko; na kuendelea na ujenzi wa miundombinu.
 
Mkakati huo unaendana na utekelezaji wa mpango wa maendeleo wa nchi hiyo ambao kwa sasa umelenga kufanya mageuzi makubwa katika taasisi za kibenki ili kuwezesha wananchi kupata mitaji ya kufanya shughuli za uchumi na maendeleo; na mageuzi ya makapuni ya biashara ya Serikali ili yaweze kushindana katika uchumi wa soko ndani na nje ya nchi pasipo kutegemea ruzuku kutoka Serikalini.‎
 
Ni dhahiri kwamba yapo mambo ambayo Tanzania inaweza kujifunza kutoka Vietnam katika safari yake ya kuwa nchi ya uchumi wa Kati ifikapo mwaka 2025. Tanzania inayo nafasi kubwa ya kuongeza uzalishaji katika mazao ya miwa,mpunga na uvuvi kwa kupitia ushirikiano na Vietnam.

Mahusiano ya Vietnam na Tanzania‎
Mahusiano ya Tanzania na Vietnam yaliyojengwa na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Kiongozi wa Vietnam Ho Chi Minh mwaka 1960 na kupelekea kuanzishwa rasmi kwa mahusiano ya kidiplomasia mwaka 1965. Kwa muda mrefu mahusiano hayo yalikuwa ya kisiasa zaidi ambapo Tanzania iliunga mkono harakati za Vietnam za kupinga uwepo wa majeshi ya kigeni kwenye ardhi yake.

Ziara za Kukuza Mahusiano za Viongozi Wakuu
Aidha katika kipindi cha miaka 50 ya mahusiano ya kidiplomasia baina ya Vietnam na Tanzania, viongozi wa kitaifa wa nchi hizi mbili wamefanya ziara za kudumisha mahusiano baina ya nchi hizi mbili. Tarehe 25 Septemba 1973, Rais wa Vietnam Mheshimiwa Nguyen Huu Tho alifanya ziara nchini Tanzania. 
 
Kwa upande wa Tanzania, viongozi waliofanya ziara nchini Vietnam ni pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Awamu ya Tatu Mhe. Benjamin William Mkapa (2004); Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Awamu ya Nne Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete (2014), Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk Ali Mohamed Shein (2012); Mawaziri Wakuu wa Serikali ya Awamu ya Nne ya Jamhuri ya Muungano‎ Mhe.Edward Lowassa (2006); na Mhe. Mizengo Kayanza Pinda (2010).

Mikataba ya Mahusiano baina ya Tanzania na Vietnam
Katika jitihada za kuimarisha mahusiano, mwaka 2001 Tanzania na Vietnam zilisaini Mkataba wa Ushirikiano wa Kuichumi na ufundi‎.  Mkataba huo uliainisha maeneo ya ushirikiano yafuatayo:
  1. Kubadilishana uzoefu katika sekta ya kilimo na maendeleo vijijini;
  2. Kubadilishana uzoefu katika matumizi ya sayansi na teknolojia katika kuendeleza kilimo cha umwagiliaji, uvuvi na misitu;
  3. Kupeana taarifa za fursa za masoko ya bidhaa za kilimo
  4. Vietnam kuipata Tanzania utaalam na teknolojia ya uvunaji na utunzaji wa maji
  5. Mwaka 2014 Tanzania na Vietnam zilisaini Mkataba wa ushirikiano katika sekta ya mawasiliano ambapo kupitia mkataba huo kampuni ya Vietel  inayomilikiwa na Jeshi la Vietnam imefanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya mawasiliano nchini na kuzalisha ajira za moja kwa moja kwa watanzania 1600 na fursa za kujiajiri kwa watanzania 20,000. Vilevile,kampuni hiyo kupitia mkataba uliosainiwa,itatoa huduma za internet bure kwenye mashule na mahospitali ya Serikali vijijini.

-Mwisho-
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Dar es Salaam
03 Machi, 2016
==

Friday, March 4, 2016

Paul Makonda Amkataa Hakimu Anayesikiliza Kesi ya Kuwakashfu Makada Wenzake wa CCM.....Kubenea Naye Akutwa na Kesi Ya Kujibu Sakala la Kumtusi Makonda



Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda jana alitinga mahakamani na kumkataa hakimu aliyekuwa akisikiliza kesi iliyofunguliwa dhidi yake na makada wawili wa zamani wa CCM wanaodai aliwakashifu.

Kesi dhidi ya Makonda, ambayo awali ilikuwa inasikilizwa na Hakimu Hellen Liwa wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, ilishafikia hatua ya utetezi na Makonda alitakiwa kuanza kujitetea jana, baada ya mahakama hiyo kumuona kuwa ana kesi ya kujibu.

Hata hivyo, jana Makonda ambaye alifika mahakamani kwa mara ya kwanza tangu kesi hiyo ilipofunguliwa, alishikilia msimamo wa kutokuwa na imani na hakimu huyo na hivyo kuomba apangiwe hakimu mwingine.

Makonda alifikia msimamo huo kutokana na maneno aliyoelezwa na wakili wake, ambayo kwa mtazamo yalionyesha kuwa hakimu atakuwa anawapendelea wadai na hivyo asingemtendea haki.

Kutokana na madai ya Makonda, Hakimu Liwa amejitoa kwenye kesi hiyo na amepanga ianze kusikiliza upande wa mashtaka Machi 23.
Kesi dhidi ya Kubenea 
Wakati Makonda akimkataa hakimu, mbunge wa Ubungo kwa tiketi ya Chadema, Saed Kubenea ameonekana ana kesi ya kujibu katika kesi inayomkabili ya tuhuma za kumtukana mkuu huyo wa wilaya. 
Uamuzi huo ulitolewa jana na Hakimu Thomas Simba wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu anayesikiliza kesi hiyo, ikiwa ni siku chache baada ya upande wa mashtaka kufunga ushahidi wake.

Akitoa uamuzi huo jana, Hakimu Simba alisema kuwa baada ya kupitia ushahidi wa upande wa mashtaka uliotolewa na mashahidi watatu, aliridhika kuwa mshtakiwa ana kesi ya kujibu.

Baada ya uamuzi huo wakili wa Kubenea, Peter Kibatala aliieleza mahakama kuwa mteja wake atajitetea kwa kiapo na kwamba watakuwa na mashahidi wanne na wanakusudia kuwaita wote mahakamani siku ya kujitetea.

Hakimu Simba alipanga mshtakiwa huyo aanze kujitetea Machi 7, mwaka huu.

Kubenea, ambaye alipandishwa kizimbani, mahakamani hapo Desemba 15, mwaka jana, anadaiwa kumtolea DC huyo lugha ya matusi Desemba 14 mwaka jana wakati wakiwa kiwanda cha Tooku Garments kilichoko Mabibo External, Kinondoni, jambo ambalo lingeweza kusababisha uvunjifu wa amani.

Anadaiwa kuwa siku hiyo alimuita Makonda kuwa ni “kibaka, mpumbavu na mjinga” na kwamba cheo chenyewe cha ukuu wa wilaya ni cha kupewa.

Wakati wa ushahidi wake, Makonda aliieleza mahakama kuwa alitumia nafasi yake ya ukuu wa wilaya kwenda kiwandani kwa lengo la kuzungumza na wafanyakazi waliokuwa wamegoma.

Mashahidi wengine wa upande wa mashtaka walikuwa ni maofisa wa polisi waliokuwapo eneo la tukio siku hiyo.

Alisema alipomaliza kuzungumza na wafanyakazi hao na kufunga kikao hicho, wakati anageuka alishangaa kumsikia mshtakiwa akimtukana.
==


Friday, March 4, 2016

Naibu Katibu Mkuu wa CUF Nassor Ahmed Mazrui Ahojiwa na Jeshi la Polisi Zanzibar Na Kuachiwa Kwa Dhamana


Wakati polisi visiwani Zanzibar wakimhoji Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Nassor Ahmed Mazrui jana, ulinzi uliimarishwa mjini Unguja huku askari wenye silaha na magari ya deraya wakifanya doria mitaani.

Mazrui, ambaye alifika makao makuu ya jeshi hilo saa 2:00 asubuhi akiambatana na wakili wake, ndiye aliyekuwa mkuu wa timu ya kampeni ya mgombea urais wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, katika uchaguzi uliofanyika tarehe 25 Oktoba 2015, ambao chama chake kinaamini kuwa kilishinda.

Barabara zinazoelekea makao makuu ya polisi kutokea Jang’ombe, Kilimani na Bomani zilifungwa huku vikosi vya ulinzi na usalama vikiwa vimetapakaa maeneo hayo na mitaa mbalimbali mjini Unguja.

Wakazi wa Zanzibar wanaojiandaa kwa uchaguzi wa marudio uliopangwa kufanyika Machi 20, kuanzia Jumatano mchana walishuhudia askari wenye sare wakiwa katika magari maalumu ya kijeshi wakirandaranda kwenye barabara za Unguja, hususan mitaa ya Ng’ambo kupitia Mnazi Mmoja, Darajani, Amani, Chumbuni na Mtoni kuelekea Bububu.

Wakati hali ikionekana hivyo mitaani, Mazrui alikuwa ndani ya Ofisi ya Upelelezi ya Makao Makuu ya Jeshi la Polisi, Ziwani mjini Unguja ambamo alihojiwa kwa saa tatu na nusu.

Alianza kuhojiwa tangu saa 2.00 asubuhi kama alivyotakiwa na jeshi hilo kuripoti kupitia barua ya wito aliyotumiwa hivi karibuni, hadi saa 5.30

Hata baada ya kumaliza kuhojiwa, Mazrui aliyekuwa waziri wa biashara, alilazimika kubaki kituoni hapo akisubiri kukamilika kwa taratibu za dhamana. Aliruhusiwa kuondoka saa 6.40 mchana.

Pamoja na ulinzi kuimarishwa, mamia ya wananchi, hasa wapenzi, wanachama na wafuasi wa CUF, walifika makao makuu ya chama hicho yaliyoko Mtendeni ili kumpokea Mazrui akitokea polisi.

Baada ya kuachiwa kwa dhamana, Mazrui alisema alihojiwa na polisi kuhusu kauli aliyoitoa hivi karibuni alipokuwa Dunga Kiembeni, Wilaya ya Kati mkoani Kusini Unguja kwamba chama chake cha CUF kimechoshwa na vitendo vya hujuma na vya kihuni dhidi ya mali na ofisi zao.

“Naam, nimewaambia kwamba hiyo ni kauli yangu na niliyesema hayo ni mimi kuwa CUF tumechoshwa na uhuni huo,” alisisitiza Mazrui mara baada ya kuachiwa kwa dhamana ya masharti ya kuwa na wadhamini wawili na kila mmoja wao kutakiwa kuweka hapo Sh500,000.

“Wamesema nimetoa kauli za uchochezi hivyo watanishtaki mahakamani na wamenitaka niripoti polisi Jumanne na Alhamisi.” Alisema
==

Friday, March 4, 2016

Naibu Waziri wa Afya Dr Kigwangala Azindua Wodi Mpya Ya Wagonjwa Mahututi Muhimbili.....Kasema Serikali ina Mpango wa Kuacha Kupeleka Wagonjwa Nje ya Nchi Kutibiwa


Serikali imesema ina mpango wa kusitisha kupeleka wagonjwa nje ya nchi kupatiwa matibabu na kuhakikisha kila kitengo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kinakuwa na chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum (ICU).

Serikali imechukua uamuzi huo, wakati taarifa ndani ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii , Jinsia, Wazee na Watoto zikieleza inadaiwa deni la Sh.28.74 bilioni za malimbikizo kutokana na ongezeko la wagonjwa wanaopelekwa nje kwa matibabu.

Akizungumza jana wakati wa kuzindua chumba cha ICU kilichopo jengo la Mwaisela hospitalini hapo, Naibu Waziri wa wizara hiyo, Dk Hamis Kigwangalla alisema lengo la Serikali ni kuanzisha vyumba hivyo kwa kila kitengo ili kupunguza vifo.

Alisema hospitali hiyo ina vitanda 25 vya ICU, lakini lengo ni kuwa na vitanda 150 vya wagonjwa mahututi na wataalamu wa kutosha.

Alisema Serikali ina mpango wa kutoa mafunzo kwa madaktari na wauguzi watakaokuwa wamebobea katika fani ya vyumba hivyo.

Madaktari na wauguzi hao watapata mafunzo kutoka Chuo Kikuu cha Cairo na mengine yatatolewa kupitia Chuo Kikuu cha Sayansi na Tiba Muhimbili (Muhas).

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa MNH, Profesa Lawrence Mseru alisema kuzinduliwa kwa ICU hiyo kunaifanya hospitali hiyo kuwa na vyumba vya aina hiyo viwili vyenye vitanda 25, kutoka chumba cha awali kilichokuwa na vitanda vinane.

Alisema uwapo wa vitanda hivyo ni ongezeko la asilimia 200 ikilinganishwa na uwezo wa awali.

“Fedha za ndani zilizotumika kwa ajili ya ukarabati wa chumba hiki ni Sh230 milioni ikiwa ni pamoja na kutafuta ufadhili kutoka taasisi isiyo ya kiserikali ya Ujerumani iliyowekeza vifaatiba vya Sh600 milioni.

‘‘Mfadhili huyu ndiye aliyetununulia vifaa vyenye thamani ya Dola 800,000 za Marekani,” alisema Profesa Mseru. 
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto, Dkt. Hamisi Kigwangalla akisisitiza jambo jana Jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi ya wodi ya ICU ilizopo kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili(MNH)
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Hosptitali ya Taifa ya Muhimbili MNH, Profesa Lawrence  Museru (katikati) akitoa maelezo mafupi jana Jijini Dar es Salaam kwa  Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya  Jamii,Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Hamisi Kigwangalla (kulia) wakati wa sherehe za uzinduzi wa wodi ya ICU iliyopo kwenye jengo la Mwaisela katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili(MNH)
Rais wa Shirika lisilo la Kiserikali la Madaktari wanaohusika na magonjwa ya ini na tumbo(Gastrenterology) kutoka Munich Ujerumani(kulia) akiteta jambo na  Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya  Jamii,Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Hamisi Kigwangalla wakati wa uzinduzi wa ICU Muhimbili.
==

Friday, March 4, 2016

Habari Zilizopo Katika Magazeti Ya Leo Ijumaa Ya March 4


==
Friday, March 4, 2016

Madaktari 2 na Wauguzi 4 Wasimamishwa kazi Jijini Mwanza Kwa Kukataa Kumzalisha Mjamzito Ambaye Alijifungua Mapacha Wawili Chooni Wakafariki



Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana mkoani Mwanza, Baraka Konisaga, amemwamuru Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, Adam Mgoyi kuwasimamisha kazi madaktari wawili na wauguzi wanne katika Hospitali ya Wilaya ya Nyamagana iliyopo Kata ya Butimba kwa kushindwa kumuhudumia mama mjamzito aliyefikishwa hospitalini hapo na kusababisha kujifungua watoto mapacha na baadaye kufariki.

Hatua hiyo imesababishwa na tukio la mgonjwa Suzana John (27) mkazi wa Kata ya Mkolani kufikishwa na ndugu zake katika Hospitali hiyo, aliyekuwa mjamzito na kupokelewa na Dk Norin Magesa na Muuguzi, Janet Foya waliokuwa zamu ya usiku siku ya Machi Mosi, mwaka huu majira ya saa 4:00 usiku na kushindwa kumuhudumia zaidi ya kutoa lugha isiyoridhisha, pamoja na uzembe.
Akielezea tukio hilo, mwanamke huyo ( Suzan John ) alidai kuwa alianza kusikia uchungu na kuomba msaada kutoka kwa madaktari na wahudumu wa afya waliokuwa hospitalini hapo bila mafanikio.
 
“Nilifika nikiwa hoi, nikawaambia muda wangu tayari  lakini hawakunisaidia zaidi ya kunitolea maneno machafu.
"Wakati muda ukizidi  kwenda huku nikiwa sipewi huduma yoyote, nilihisi kubanwa haja ndogo hivyo nikaamua kwenda chooni .
Kule chooni mambo yakabadilika ghafla, mtoto wa kwanza akawa keshaanza kutoka.Bahati nzuri mle chooni kulikuwa na beseni
"Nililichukua lile beseni kwa ajili ya kuwaweka watoto huku niwakaita manesi.Manesi hao walikuja wakanichungulia halafu wakarudi. Akaja Nesi mmoja mwanafunzi, akakata kitovu akawaweka kwenye nguo, wakawa wamefariki,” Bi. Suzan alieleza kwa uchungu huku akilia.
Baada  ya mapacha hao kufariki, ndugu wa mwanamke huyo pamoja na wagonjwa wengine walioshuhudia mkasa huo walipandwa na hasira huku wakitaka kuwapiga wauguzi hao.
Taarifa za vurugu hizo zilimfikia DC Konisaga ambaye alifika hospitalini hapo  na kukutana kwa dharula na Mkurugenzi wa Jiji, Adamu Mgoyi, baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya ya Nyamagana, Kaimu Mganga Mkuu Mkoa, Uongozi wa Hospitali na baadhi ya ndugu wa mgonjwa Suzana John aliyejifungua watoto mapach.

Katika kikao hicho cha dharura, walipokea maelezo ya pande mbili, kutoka kwa wauguzi na familia ya mgonjwa Suzana, na kupitia taarifa zilizokuwa zimeandikwa na Madaktari wawili waliomuona mgonjwa huyo, ndipo DC Konisaga akamuagiza Mkurugenzi Mgoyi na Kaimu Mganga Mkuu kuwasimamisha kazi madaktari wawili na wauguzi wanne ili kupisha uchunguzi wa kitaalamu juu ya tukio hilo.

Konisaga aliwataja wanaotakiwa kusimamishwa kazi kuwa ni Dk Magesa na muuguzi Foya waliompokea mgonjwa wakiwa zamu ya usiku wa Machi Mosi, mwaka huu na kushindwa kumpatia huduma zaidi ya kumtolea lugha chafu na uzembe huku wakishindwa kutoa maelezo wakati wa kukabidhi majukumu kwa madaktari na wauguzi walioingia zamu ya asubuhi ya Machi 2, mwaka huu.

DC Konisaga pia alieleza kuwa pamoja na kuingia kwa madaktari na wauguzi wa zamu ya asubuhi ya Machi 2, bado hawakumjali na kumhudumia mgonjwa huyo huku baadhi wakitoa lugha zisizo za faraja kwa ndugu wa mgonjwa. 
Hata alipozidiwa na kupewa taarifa na ndugu wa mgonjwa huyo, hawakufika na mara kadhaa walikuwa wakifika na kutoka bila kumudumia pamoja na kumsikiliza akilalamika.

Aliwataja wengine wanaotakiwa kusimamishwa kazi mara moja ni Dk Emiliana Mvungi, wauguzi ni Maria Mkankule, Suzana Sindano na Bibiana Moshi ambao walikuwa zamu na kutomhudumia mgonjwa ambaye alijifungua katika mazingira hatarishi akiwa Hospitalini hapo.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Magesa Mulongo amemwagiza Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Dk Rweyendela Onesmo ambaye ni Mganga Mkuu Mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa ya Sekou -Toure kupewa maelezo ya kina kutoka kwa Mganga Mfawidhi wa Hospitali hiyo, Dk Nangi William na Mganga Mkuu wa Jiji, Dk John Andrew juu ya kushindwa kuchukua hatua pamoja na kupewa taarifa hizo.

Mulongo pia amemuagiza Dk Onesmo kuunda tume ya uchunguzi itakayoshughulikia suala la tukio hilo na kisha kukamilisha kazi hiyo kwa siku moja na kumpatia taarifa ili hatua kali za maadili ya utumishi wa umma zichukue mkondo wake ili pia kuwezesha kusaidia jinsi ya kuboresha utendaji wa kitaalamu na kitabibu katika hospitali hiyo ambayo kwa muda mrefu imekuwa ikilalamikiwa na wananchi kutokuwa na huduma nzuri kwa wagonjwa.
==